Wednesday, March 11, 2015

Video ya Kumbukumbu ya Miaka Kumi ya Kitabu

Jana, binti yangu Zawadi na mimi tulirecodi video ya kumbukumbu ya miaka kumi tangu nilipochapisha kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Hatukuwazia tungefanya shughuli hiyo jana. Tulijishitukiza bila maandalizi. Tulitayarisha kompyuta nami nikaanza kuongea. Zawadi alifanya shughuli yote ya kiufundi hadi kuiweka video katika
mtandao wa You Tube.

Katika kumbukumbu hii ya miaka kumi ya kitabu changu, napenda kuwashukuru wasomaji wangu, familia, na marafiki na wengine wote walionihamasisha kwa namna moja au nyingine.

Kwa mwezi huu wote, yeyote anayetaka kitabu hiki, popote duniani, ataweza kukipata kutoka kwangu kwa bei nafuu ya dola 12. Awasiliane nami kwa barua pepe, africonexion@gmail.com au simu (507) 403 9756. Mwisho wa fursa hii ni tarehe 31.

Tuesday, March 10, 2015

Mdau Anauliza Kama Ufisadi Utaisha Nchini

Mdau anonymous ameomba tusome makala ifuatayo na ameuliza iwapo ufisadi utaisha Tanzania.

Makala aliyoleta inamhusu Dr. Fulgence Mosha, anayeonekana pichani, daktari bingwa mstaafu wa hospitali ya KCMC, ambaye amekuwa akihangaikia mafao yake ya ustaafu kwa miaka kumi bila mafanikio. Makala aliyoileta mdau ni hii hapa.

Sunday, March 8, 2015

Natamani Kuwatukana Akina "Anonymous"

Katika blogu kuna maudhi ya aina aina. Wanaoleta maudhi hayo ni hao wanaojiita "anonymous." Kwa kujificha namna hii, wanajisikia huru kusema cho chote, wakijua kuwa hakuna atakayewawajibisha.

Siku chache zilizopita, niliandika ujumbe katika blogu ya Michuzi, nikiulizia kuhusu taratibu za ibada ya mazishi ya ki-Katoliki. Sikujificha. Kama ilivyo kawaida yangu, nilijitambulisha kikamilifu.

Walitokea akina "anonymous" wakaongelea mambo ambayo hayakuonyesha nia ya kujibu suali nililouliza. Nilivyokuwa nasoma waliyoandika, niliona kuwa wananipotezea muda. Walikuwa wanakera. Kwa silika za kibinadamu, nilitamani kuwatukana, lakini niliamua kuachana nao, nikahamishia mada yangu katika blogu yangu.

Kwanza, sidhani kama ni uungwana kuingia katika blogu ya mtu na kuigeuza kuwa uwanja wa malumbano yasiyo na tija au ya kuwakera watu. Ni kama kukaribishwa nyumbani mwa mtu halafu uanze kufanya utovu wa heshima.

Miaka kadhaa iliyopita, Michuzi alilalamika kuhusu watu waliokuwa wanafanya utovu wa nidhamu katika blogu yake. Hadi leo, ameweka angalizo kuwa mchangiaji aangalie asichafue hali ya hewa wala kujeruhi hisia za mtu au watu.

Mimi mwenyewe nimekumbana tena na tena na akina "anonymous" wasio na uungwana. Kwa mfano, "anonymous" mmoja aliwahi kuniambia kwa kiburi kuwa ana uhuru wa kusema katika blogu yangu.

Napingana na "anonymous" huyu. Ingawa binafsi nimejiamulia kuifanya blogu yangu iwe huru kwa yeyote kutoa maoni yake, lakini sikubali kwamba yeyote ana haki ya kuandika katika blogu yangu.

Mtu anapokuja katika blogu yangu ninamwona kama mtu ninayemkaribisha nyumbani mwangu. Hawezi kudai kuwa ana uhuru kusema lolote atakalo katika nyumba yangu. Lazima atumie busara.

Mwenye nyumba ana haki ya kumtolea nje yeyote asiyeheshimu nyumba. Hivyo hivyo, nina haki ya kumzuia mtu yeyote kuweka maoni yake katika blogu yangu. Ninaweza kutumia njia iliyopo katika muundo wa blogu ya kuzuia maoni au kuondoa maoni.

Kwa hiari yangu, nimeamua kutotumia utaratibu huu wa kuzuia au kuondoa maoni. Lakini mtu asiniambie kwamba ana haki ya kutoa maoni katika blogu yangu.

Hii si mara yangu ya kwanza kuwaongelea akina anonymous wanaokera. Mara ya kwanza, niliandika makala hii hapa. Baadaye niliandika makala hii hapa.

Sijui wanablogu wenzangu wana maoni gani. Sijui wanaoandika au wanaowazia kuandika katika blogu wana maoni gani. Sijui wasomaji wa blogu wanasemaje.

Thursday, March 5, 2015

Kofia Katika Mazishi ya Ki-Katoliki

Niliona taarifa za msiba na mazishi ya Kapteni John Komba mitandaoni. Ni jambo la kushukuru kwamba waandishi na wapiga picha walituwezesha tulio mbali kuelewa mambo yalivyokuwa.

Nilivyoona picha inayoonekana hapa kushoto, ya jeneza likiteremshwa kaburini, niliamua kuandika ujumbe katika blogu ya Michuzi nikisema kuwa nimekerwa na kitendo cha wahusika kuwa wamevaa kofia wakati wa shughuli hiyo. Niliuliza iwapo jambo hili linaruhusiwa kwa mujibu wa ibada za mazishi ya ki-Katoliki.

Akina "anonymous" kadhaa wamejitokeza na kuandika hili au lile, katika sehemu ya maoni. Nami katika sehemu ile ya maoni, nimejaribu kuelezea zaidi suala langu, nikisema, kwa mfano, kuwa kwa askofu kuvaa kofia ya kiaskofu wakati wa kuendesha ibada ni sehemu ya mavazi yake rasmi ya ibada.

Sikuona kama duku duku yangu imejibiwa. Badala yake, niliona watu wanazua mambo ambayo hayahusiani na ulizo langu, ulizo ambalo lilitokana na nia njema, yaani kujiridhisha kuwa tunaheshimu ibada na tunamheshimu marehemu.

Nimeamua kuhamishia suali langu hapa kwenye blogu yangu. Ningependa kusikia maoni ya wa-Katoliki wenzangu, ambao wana ufahamu zaidi yangu kuhusu uvaaji wa kofia wakati wa ibada ya mazishi ya ki-Katoliki.

Tuesday, March 3, 2015

Utamaduni wa Kuwasomea Watoto Vitabu

Nimeandika mara kwa mara kuhusu suala la elimu, sio tu katika blogu hii, bali pia katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, kitabu ambacho nilitegemea kitasomwa na wa-Tanzania wenzangu, lakini mambo yamekuwa kinyume.

Kati ya mambo ambayo nimekuwa nikiyaongelea ni umuhimu wa kuwasomea watoto vitabu, jambo ambalo limejengeka katika utamaduni wa wa-Marekani. Nimekumbuka yote hayo leo baada ya kusoma makala hii hapa
kama uthibitisho na changamoto.

Hili ni kati ya mambo ambayo wa-Tanzania tunapaswa kujifunza. Nimethibitisha mwenyewe kuwa watoto wa Tanzania wanapenda vitabu, bali, kadiri wanavyokua, mapenzi hayo huzimishwa na watu wazima na jamii kwa ujumla.

Kama wahenga walivyosema, mtoto umleavyo ndivyo akuavyo. Baada ya muda, watoto wa ki-Tanzania hufuata utamaduni wa jamii wa kutothamini vitabu, na Taifa linaendelea kuzorota kielimu., wakati wenzetu wa-Marekani wanawalea watoto wao katika kupenda vitabu.

Mwalimu Nyerere alikuwa mstari wa mbele katika kuwahamasisha watu wawe na tabia ya kutafuta elimu. Alikuwa mwandishi na msomaji makini. Alionyesha mfano kwa vitendo. Aliongoza njia.

Leo tuna watu ambao tunawaita viongozi ambao sielewi kwa nini wanaitwa viongozi. Wangekuwa ni viongozi, wangetambua kuwa elimu ni msingi wa maisha na maendeleo. Wangekuwa wanaihamasisha jamii kwa kauli na vitendo katika kutafuta elimu. Lakini, badala yake, hawaonekani kujali kabisa kwamba wanachangia katika kuliangamiza Taifa badala ya kuliongoza, yaani kulipeleka mbele.

Monday, March 2, 2015

Nimeulizwa Inakuwaje Siuzi Vitabu Vyangu Tanzania

Leo katika mtandao wa Facebook kuna mdau kaniuliza inakuwaje siuzi vitabu vyangu Tanzania. Nimemshukuru kwa ulizo lake, nikajaribu kulijibu. Napenda kuandika machache kuhusu suali hili.

Napenda kuanza kwa kusema kuwa vitabu hivyo vinapatikana mtandaoni, kama vile kwenye tovuti ya lulu na tovuti ya Amazon. Yeyote mwenye kadi ya "credit" kama vile VISA au MasterCard, anaweza kuvinunua. Haijalishi kama yuko Chake Chake, Dar es Salaam au Tukuyu. Ataletewa. Kama ana kifaa kama "kindle," ananunua bila tatizo.

Ninafahamu kuwa ni wa-Tanzania wachache walioko Tanzania wanaoweza kununua vitu mtandaoni. Lakini kuna maelfu ya wa-Tanzania katika nchi kama Marekani wenye hizo kadi. Kama kuna nia ya dhati ya kununua kitabu, haikosekani njia.

Mimi mwenyewe nimekuwa tayari kufanya mipango na wa-Tanzania wenye nia ya kuuza vitabu vyangu, kwa kuwapelekea. Nimewahi kufanya hivyo na Cultural Tourism Program (Longido), Bougainvillea Lodge (Karatu), na Cultural Tourism Program (Mto wa Mbu).

Kila inapowezekana, nafanya mpango wa kuvifikisha vitabu vyangu kwenye matamasha nchini Tanzania, kama ilivyoelezwa hapa.

Kwa kuwa mimi si mfanyabiashara, ningependa kuona wafanyabiashara wanajipatia faida kutokana vitabu vyangu. Duka la vitabu chuoni St. Olaf linauza vitabu vyangu kwa bei kubwa kuliko mtandaoni. Vile vile, nilipotembelea chuo cha South Central, katika duka la vitabu walikuwa wanauza kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kwa dola 17.95.

Hata hivi, huwa najiuliza ni wa-Tanzania wepi wanaotaka kusoma vitabu vyangu. Sijaona kama kuna utamaduni wa kununua na kusoma vitabu. Wa-Marekani ndio wasomaji wangu wakuu, kama ninavyobainisha mara kwa mara katika blogu hii. Kwa vyovyote, kuepusha lawama, na kuwatendea haki wa-Tanzania wanaoamini nina jambo la kuwaambia, najitahidi kuhakikisha vitabu vyangu vinapatikana Tanzania.

Sunday, March 1, 2015

Imekuwa Wiki ya Mafanikio

Wiki hii inayoisha imekuwa ya mafanikio makubwa kwangu. Napenda kwanza nifafanue kuwa dhana yangu ya mafanikio ni tofauti na ya wale wanaowazia fedha. Mimi ni mwelimishaji, darasani na katika jamii. Ni mtoa ushauri katika masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake, hasa katika dunia ya tandawazi wa leo. Ushauri huo natoa kwa njia mbali mbali, hasa maandishi na mazungumzo na watu binafsi au vikundi. Dhana yangu ya mafanikio imejengeka katika shughuli hizo.

Kwanza, nilijiandaa kwa ziara ya chuo cha South Central, mjini Mankato, ambako nilifanya mazungumzo na darasa la wanafunzi wanaojiandaa kwenda Afrika Kusini kimasomo, na halafu nikatoa mhadhara kwa wanajumuia hapo chuoni, ambao mada yake ilikuwa "Writing About Americans."

Maandalizi ya mazungumzo hayo yote yalikhusu kukusanya fikra zilizokuwa akilini mwangu na kuziweka pamoja ili kukidhi mahitaji ya mazungumzo yale. Ilikuwa rahisi kujitayarisha kwa maongezi na wanafunzi waendao Afrika Kusini. Nmaongezi ya aina hiyo na wa-Marekani wengi katika maandalizi ya kwenda Afrika.

Katika kuandaa mhadhara wa "Writing About Americans," nilijikuta ninatafakari namna ya kuwasilisha mada yangu. Hatimaye, niliamua kuzingatia uzoefu wangu wa kuandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Niliamua nielezee chimbuko la wazo na azma ya kuandika kitabu hicho, mchakato wa kuandika, na mambo niliyojifunza katika kuandika huko. Baada ya kuamua hivyo, nilikaa chini nikatmia dakika chache tu kuandika dondoo ambazo ningetumia katika mhadhara.

Nilipoziangalia dondoo hizo, nilijua kwa hakika kwamba nitatoa mhadhara mzuri. Na ndivyo ilivyokuwa, kama alivyoeleza Mwalimu Becky Fjelland Davis katika blogu yake. Baada ya ziara yangu, niliandika katika blogu yangu kwamba nilitegemea kuwa tathmini ya ziara yangu ingeendelea miongoni mwa wale waliohidhuria.

Ukweli wa dhana yangu umeendelea kujitokeza, na hapa napenda kuleta ujumbe ulioandikwa na mtu aliyehudhuria mhadhara wangu:

Dr. Mbele,

I attended the talk you gave at South Central and found it to be very interesting and insightful. You showed how valuable writing is in itself, by giving us a mirror of ourselves as authors.

Thank you for your willingness to share you observations of Africans and Americans as well as your own self-assessments.

I thoroughly enjoyed your talk and only wish that I could have remained loner to hear the questions from the audience.

Thank you for sharing your life and writing experiences with us at South Central College
.

Baada ya ziara ya Mankato, nilijikuta nikiongea kwa njia ya Skype na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Montana, ambao walikuwa wanasoma kitabu changu cha Matengo Folktales. Niliandika kuhusu mazungumzo hayo katika blogu hii. Mazungumzo yale yalikwenda vizuri sana. Wanafunzi na mwalimu wao walifurahi, na mimi pia.

Wameendelea kuelezea furaha yao. Mwanafunzi mmoja ameniandikia hivi:

Hello Dr. Mbele!

I was a student from Professor Olsen's Skype class earlier today, my name is Sara Saxton. I'm I just wanted to say thank you so much for your time and expressing your mind to our class! I really enjoyed hearing about your definition of a classroom. I agree with the aspect of having a classroom be a "safe place" for learning. I feel as though I have experienced many things outside of the classroom, but there is nothing that compares to being able to ask questions you've always wanted to ask in a classroom. Anyway, I just wanted to let you know I really enjoyed hearing about your tales and watching you preform them. It was great!

Thank you again
!!

Mwanafunzi mwingine kaniandikia hivi:

Shikamoo Dr. Mbele,

I hope I have used the greeting properly. I wanted to say thank you taking the time to speak with, and preform for our class today over Skype. Growing up in Montana there are not many oppertunities to experience the vastness of culture the world has to offer and your time and knowledge was greatly appreciated. I hope to have the chance to speak with you again someday.

Asante sana
!

Kama ninavyosema mara kwa mara, blogu yangu hii ni mahali ambapo nahifadhi mambo yangu, kama vile mawazo, hisia na kumbukumbu. Nafurahi nimeandika hayo niliyoandika, muhtasari wa mafanikio niliyoyapa wiki hii inayoisha. Ni mafanikio yanayougusa moyo wangu na yenye maana kwangu kuliko fedha.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...