Saturday, February 14, 2015

Miaka Kumi ya Kitabu: Shukrani Wanablogu

Katika kusherehekea miaka kumi tangu nilipochapisha kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nawajibika kuwakumbuka watu wengi waliokuwa nami bega kwa bega katika kunitangazia kitabu hiki. Leo napenda kuwakumbuka wanablogu wa ki-Tanzania, ambao wamechangia katika kunihamasisha na kuniunga mkono miaka yote hii.

Pichani hapa kushoto anaonekana mwanablogu Simon Kitururu, ambaye amewahi kuniambia mara kadhaa kuwa anasoma maandishi yangu kila yanapopatikana. Anaonekana ameshika vitabu vyangu viwili: Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Picha hiyo aliichapisha katika blogu yake ya Mawazoni.

Mwanablogu Issa Michuzi amefanya juhudi kubwa kutangaza shughuli zangu, kama vile warsha na mihadhara. Ni mfuatiliaji wa blogu yangu, na mara kwa mara huamua kuchapisha baadhi ya makala zangu katika blogu yake. Hata leo amechapisha makala yangu kuhusu kitabu changu kutimiza miaka kumi.

Subi Nukta naye ametoa mchango wake, ikiwemo kutangaza kitabu hiki kinachotimiza miaka kumi. Katika blogu yake, aliandika hivi:

Africans and Americans: Embracing Cultural Differences is a book by Professor Joseph Mbele that I would recommend to anybody willing to learn something about a culture that is different fro theirs.

Since Tanzania is my home country, I'd ask anybody planning to travel to Tanzania, or anybody unsure on what to do when in a different culture to buy this book. To order your copy, simply click on the book's image and you will be taken to lulu.com where you can purchase it
.

Jeff Msangi ni mwanablogu mwingine ambaye ananiunga mkono kwa dhati. Aliandika kuhusu kitabu changu hapa. Hakuishia hapo, bali siku nyingine alandika hivi:

Now, if you live or have lived in the US in the past, you will agree with me that there are a lot of things or let me call them cultural differences between Africans and Americans. There is a lot of learning and adjustment for newcomers/immigrants from Africa. The same applies to Americans going or rather growing up in Africa. My good friend, Prof. Joseph Mbele, highlights these cultural differences very well in his famous book titled “Africans and Americans-Embracing Cultural Differences”. I recommend everyone to read this book.

Christian Bwaya ameandika mara kadhaa kuhusu kitabu hiki, kwa mfano hapa. Wanablogu wengine wametoa mawazo yao kuhusu kitabu hiki katika maoni kwenye mijadala. Mfano ni Sophie Becker ambaye aliandika katika blogu ya Jielewe:

Hiki kitabu kifundisha na kuburudisha. Kinakuelezea mambo ambayo yangekuchukua miaka kadhaa kuyaelewa au usiyaelewe kabisa harafu Prof.Mbele kakiandika with sense of humor utacheka sana.nimekipenda sana.

Ningeweza kuendelea kuwataja wanablogu wengine, kama vile Rachel Siwa Isaac, Profesa Masangu Matondo, na Yasinta Ngonyani, ambaye aliandika maoni yake hapa. Naamini kuwa wanablogu niliowataja na hata ambao nimeshindwa kuwataja, hawajaishia kuandika tu kuhusu kitabu changu. Bila shaka, kama ilivyo ada kwetu wanadamu, wamekiongelea na wanakiongelea katika mazingira mengine pia, kwa marafiki na watu wengine. Ninawashukuru wote kwa kuniunga mkono katika jukumu hili la kujenga mahusiano mema baina ya watu wa tamaduni tofauti.

Thursday, February 12, 2015

Kitabu Kimetimiza Miaka Kumi

Kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimetimiza miaka kumi tangu nilipokichapisha, tarehe 5 Februari, mwaka 2005. Siku hiyo niliuingiza muswada katika mtandao wa lulu nikalipia namba ya utambulisho wa kitabu, yaani ISBN. Siku hiyo hiyo niliagiza nakala ya kwanza, nikaipata baada ya wiki moja hivi. Wiki hii ni kumbukumbu ya miaka kumi ya kuwepo kwa kitabu hiki.

Mambo mengi yametokea katika miaka hii kumi kuhusiana na kitabu hiki. Nimepata fursa ya kusikia maoni ya wasomaji wengi. Baadhi wameandika maoni hayo na kuyachapisha, kama vile katika tovuti, blogu, na majarida. Wengine wameniandikia maoni yao katika barua pepe. Wengine wamenieleza maoni yao katika maongezi ya ana kwa ana.

Watu waliotoa maoni yao kuhusu kitabu hiki ni wa aina mbali mbali. Baadhi nawakumbuka vizuri, kama vile Mhashamu Askofu Owdenburg Mdegella wa dayosisi ya Iringa ya Kanisa la Kiluteri Tanzania, ambaye alisema kuwa kitabu kimemfurahisha sana na anataka wageni wakisome ili watuelewe wa-Tanzania. Aliniambia hayo siku tulipokutana kwenye chuo cha Peace House, Arusha, na alikuwa anaongea kutokana na uzoefu wake mkubwa wa kuwapokea na kushughulika na wa-Marekani wanaokuja Tanzania katika mpango wa ushirikiano baina ya waumini wa-Marekani na wa-Tanzania uitwao Bega kwa Bega.

Mwingine ninayemkumbuka vizuri ni Balozi Mstaafu Andrew Daraja. Alikisoma kitabu hiki wakati akiwa balozi wa Tanzania hapa Marekani, na alinipigia simu akaniambia jinsi alivyokipenda kitabu hiki kama nyenzo ya kuweka maelewano baina wa wa-Marekani na sisi wa-Afrika.

Mzee Patrick Hemingway, katika maongezi naye, amekuwa akikisifia kitabu hiki. Siku tulipomtembelea, alisema kuwa kitabu hiki ni "tool of survival." Mzee huyu m-Marekani anajua anachokisema, kwani aliishi Tanganyika (baadaye Tanzania) kwa miaka yapata 25. Ninaguswa na maoni ya watu kama yeye, ambao wanajua hali halisi ya tofauti baina ya utamaduni wao na wetu.

Katika miaka hii kumi, nimepata mialiko kadha wa kadha kutoka kwenye vyuo, taasisi, makampuni, na vikundi, kwenda kutoa mihadhara kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake. Ingawa kitabu hiki ni kifupi tu kilichoandikwa kwa lugha rahisi, wala si cha kitaaluma, kimenisaidia kuendesha mihadhara hiyo na pia warsha, na hata kutatua migogoro ya kutoelewana baina ya wa-Marekani na wahamiaji na wakimbizi kutoka Afrika.

Ninawashukuru kwa namna ya pekee watu waliochangia kwa namna moja au nyingine kwa kukisoma kitabu, kuwaelezea wengine, na kunipa maoni yao. Wiki hii nitawakumbuka kwa namna ya pekee.

Mambo ni mengi sana yaliyotokea katika miaka hii kumi, ambayo ningeweza kuyaandikia kitabu. Panapo majaliwa, nitafanya hivyo.

Sunday, February 8, 2015

Mwenyeji Wetu Longido, Tanzania

Picha hii ilipigwa Januari, 2013, nilipokuwa Longido, Tanzania. Niko na Ndugu Ally Ahamadou, mkurugenzi wa programu ya utalii wa utamaduni hapa Longido. Yeye ndiye alikuwa mwenyeji wa misafara yangu katika kozi kuhusu safari na maandishi ya Ernest Hemingway.

Programu ya utalii wa utamaduni Longido ni moja kati ya programu maarufu za aina hii nchini Tanzania. Taarifa kuhusu program hii zinapakana kirahisi mtandaoni.

Binafsi nimeshuhudia jambo hili kwa jinsi makala niliyochapisha katika blogu yangu ya ki-Ingereza kuhusu utalii wa utamaduni Longido inavyotembelewa na wasomaji wengi. Hali hii imenithibitishia kuwa blogu inaweza kuwa nyenzo yenye uwezo mkubwa wa kutangaza utalii.

Ingawa Ndugu Ally Ahmadou si mzaliwa wa Longido, bali Tanga, niliona anakubalika sana na watu wa Longido. Hata kwa kuongea naye muda mfupi tu, unapata picha kuwa huyu ni mpenzi Longido na shughuli za utalii wa utamaduni. Programu hii ya utalii wa utamaduni Longido niliona inapendwa na watu wa Longido, kwa kuwa faida zake katika jamii yao wanaziona.

Ndugu Ally Ahmadou nilimwona kuwa mtu mwepesi wa kuangalia fursa mpya katika shughuli ya utalii. Mfano ni jinsi tulivyoongelea suala la vitabu katika utalii, suala ambalo nimeliongelea katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii na nililigusia pia katika blogu hii. Ndugu Ally alipofahamu kuwa nimechapisha vitabu vinavyoweza kuchangia katika sekta hiyo, alichukua nakala za kutosha za Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kwa ajili ya watalii ambao wangependa kuvinunua.

Thursday, February 5, 2015

Kitabu Kimemgusa Mdau wa Bangladesh

Leo asubuhi nimepigiwa simu na mama mmoja kutoka Bangladesh anayefanya kazi katika benki ninayoitumia. Wiki kadhaa zilizopita, baada ya kufahamu kuwa hakuwa amekaa sana hapa Marekani, nilimwazimisha nakala ya kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ili aone mambo yalivyokuwa kwangu katika utamaduni huu mgeni. Nilihisi kuwa kingemsaidia kwa namna moja au nyingine.

Siku nyingine, nilipokwenda benki kwa shughuli zangu, tulionana, na aliniambia kuwa kitabu amekipenda, ila kilikuwa nyumbani. Basi nilimwambia kuwa tutafanya mpango nikichukue siku nyingine.

Jana nilimpigia simu kazini kwake, na kwa vile hakuwepo, niliacha ujumbe kwenye simu kwamba ninashiriki maonesho Jumamosi hii na, ikiwezekana, ningechukua kile kitabu; la sivyo, akitaka, anaweza kukilipia katika akaunti yangu na kukichukua moja kwa moja.

Leo asubuhi amenipigia simu, tukaongelea suala la kitabu. Alisema amekipenda na angetaka kumpelekea kaka yake aliyeko Canada, ila sasa hajui itakuwaje kwa vile ninakihitaji kwenye maonesho. Nilimwambia kuwa nina nakala zingine ambazo nadhani zitatosha, naye alisema atalipia kitabu. Nilimshukuru, nikamwuliza iwapo tutaweza kupanga siku tukutane, ili anieleze mawazo yake kuhusu yaliyomo kitabuni. Alikubali hima.

Nimeona niandike kumbukumbu hizi, kama ilivyo kawaida katika hii blogu yangu. Tangu siku ya kwanza mama huyu aliponiambia kuwa kitabu amekipenda, nilitambua kuwa ingawa niliandika kuhusu utamaduni wa mu-Afrika, kitabu kinawagusa watu wasio wa-Afrika pia.

Hili halikuwa jambo la ajabu kwangu, kwani katika kufundisha fasihi za sehemu mbali mbali za dunia, napata fursa ya kuyaelewa mambo kadha wa kadha ya tamaduni hizo. Nimegusia jambo hilo katika utangulizi wa kitabu changu.

Hata hivi, ingawa kusoma fasihi kutoka nchi fulani ni fursa ya kuufahamu utamaduni wa nchi ile, kuongea ana kwa ana na mtu au watu wa nchi ile ni fursa ya aina yake. Nami nangojea kwa hamu kuongea na huyu mama wa Bangladesh kuhusu kitabu changu na utamaduni wa kwao. Ninahisi nitajifunza mengi.

Wednesday, February 4, 2015

Wanachuo wa Gustavus Adolphus, Marekani, Wameifurahia Tanzania

Wanachuo wa Chuo cha Gustavus Adolphus, ambao walikuwa Tanzania mwezi Januari mwaka huu kwa ziara ya kimasomo, wamerejea salama nchini kwao Marekani. Hao ni wale ambao niliongea nao kuhusu tofauti baina ya utamaduni wa Marekani na ule wa kwetu Afrika, katika kuwaandaa kwa safari.

Jana, mmoja wao ameandika ujumbe katika blogu yangu ya ki-Ingereza:

Dr. Mbele,
Thank you very much for meeting with us before we left for Tanzania. We had a wonderful trip and learned so much about the differences and similarities between our two cultures. The Tanzanians are a beautiful people-- so full of happiness and passion for life. I will never forget my time there and hope that I can go back someday! Thanks you also for signing my copy of your book.
Abby Simms


Natafsiri ujumbe huu hivi:

Dr. Mbele,
Asante sana kwa kukutana nasi kabla hatujaondoka kwenda Tanzania. Safari yetu ilikuwa nzuri sana, na tulijifunza mengi kuhusu jinsi tamaduni zetu mbili zinavyofanana na jinsi zinavyotofautiana. Wa-Tanzania ni watu wazuri--wamejaa furaha na ari ya maisha. Sitasahau kamwe muda niliokuwepo kule na natumaini siku moja kwenda tena! Asante pia kwa kusaini nakala yangu ya kitabu chako.
Abby Simms.


Niliandika katika blogu hii kuwa hao wanachuo, kama walivyo wa-Marekani wengine, wana tabia ya kuripoti kuhusu safari na kukaa kwao Tanzania, nikaahidi kuwa nitakavyopata ripoti hizo, nitaziweka hapa katika blogu yangu.

Sidhani kama kuna m-Tanzania ambaye hatafurahi kusoma ripoti kama hii ya Abby Simms, kwa jinsi inavyotukumbusha kuwa tunayo mema na mazuri. Tukiamua, tunaweza kujibadili tukaachana na yale mabaya na tukaendeleza yale mema na mazuri.

Tuesday, February 3, 2015

Wa-Marekani na wa-Tanzania: Tofauti za Tamaduni

Leo, katika ukurasa wake wa "Facebook," Ndugu Maggid Mjengwa aliandika: "Leo Nimepokea Wafanyakazi Wa Kujitolea Kutoka Marekani..."

Wa-Marekani hao, ambao anaonekana nao katika picha hapa kushoto, wamefika Iringa kujitolea katika Kwanza Jamii, kampuni inayoendesha gazeti na redio. Maggid hakutuambia watakaa muda gani hapo Iringa, lakini nilijibu ujumbe wake "Facebook" namna hii:

"Safi sana. Ninapoona au kusikia mambo ya aina hii, wazo linalonijia akilini ni kuwa muhimu wageni wapate mtu wa kuwaelezea angalau yale ya msingi kuhusu tofauti kati ya utamaduni wa-Marekani na ule wa wa-Bongo, na wa-Bongo pia waelezwe kuhusu tofauti kati ya utamaduni wao na ule wa wa-Marekani. Hii ni kwa ajili ya kurahisisha shughuli na maisha kwa pande zote mbili. Kila la heri."

Suala hili nililoongelea ni muhimu hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Hao wageni wanapokuja kwetu na sisi tunapoenda kwenye nchi zao, ni mihumu kulizingatia, ili kufanikisha shughuli na mahusiano baina yetu. Nimeandika kuhusu tofauti baina ya utamaduni wa wa-Marekani na wa-Afrika katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho nashukuru kwa jinsi kinavyowasaidia watu wanaokisoma, kama ilivyoelezwa hapa na hapa.

Hilo ni suala ninalolishughulikia sana katika utafiti, mihadhara na warsha. Hiyo picha hapa juu tayari inanipa vidokezo muhimu. Ninaona jinsi hao wasichana walivyomwangalia Maggid usoni, na yeye ameangalia chini. Hapo Mjengwa anaonyesha heshima kwao, kwa mujibu wa utamaduni wetu wa ki-Tanzania na ki-Afrika kwa ujumla.

Nao hao wasichana, kwa mujibu wa utamaduni wa Marekani, wanaonysha heshima kwa kumwangalia Maggid usoni. Huenda wanashangaa kwa nini hawaangalii usoni. Hilo suala la kuangaliana usoni ni moja ya yale ninayoyaongelea katika kitabu changu:

Kama hii picha ingekuwa ni video, ingenipa fursa ya kusema mengi zaidi.

Sunday, February 1, 2015

Uandishi ni Kazi ya Upweke

Waandishi kadhaa maarufu wametamka kuwa uandishi ni kazi ya upweke. Mmoja wa waandishi hao ni Ernest Hemingway, ambaye picha yake inaonekana hapa kushoto.

Katika hotuba yake ya kupokea tuzo ya Nobel, alisema:

Writing, at its best, is a lonely life. Organizations for writers palliate the writer's loneliness but I doubt if they improve his writing. He grows in public stature as he sheds his loneliness and often his work deteriorates.

Najaribu kuitafsiri kauli hii:

Uandishi, katika hali yake bora kabisa, ni maisha ya upweke. Vyama vya waandishi hupunguza upweke wa mwandishi lakini sidhani kama vinaboresha uandishi wake. Hadhi yake katika jamii hukua kwa kadiri anavyoupunguza upweke wake na aghalabu ubora wa kazi yake hudorora.

Hemingway alilitafakari na kuliongelea sana suala la uandishi. Alifanya hivyo katika riwaya, insha na barua zake na pia katika mahojiano na maongezi mengine. Nami ninajifunza mengi kutoka kwake.

Katika makala yangu ya juzi nilitamka kwamba ninapoandika katika blogu yangu hii, ninajiandikia mwenyewe. Sijui na sijali kama kuna atakayesoma ninachoandika. Lengo langu la msingi ni kutimiza haja yangu ya kuutua mzigo uliokuwepo mawazoni mwangu.

Ni wazi kuwa fikra yangu hii inahusiana na yale ninayojifunza kutoka kwa Hemingway. Siko tayari kusukumwa na imani kwamba ninaiandikia jamii. Ningependa kuzingatia kauli ya Hemingway kwamba, "Writing, at its best, is a lonely life."

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...